THTU inasimama kama Tanzania Higher Learning Institutions Trade Union kwa Kiswahili Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania. THTU ni chama kilicho sajiliwa tarehe 12/12/2008 na kupata usajili Na. 23 (reg.23) chini ya sheria inayosajili vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, Na.6 ya mwaka 2004). THTU inajumuisha wafanyakazi wa vyuo vikuu, Vyuo vikuu vishiriki, Taasisi za Elimu ya Juu na Taasisi zinazosimamia Elimu nchini Tanzania.
Hapa kwetu SUA taarifa za uanzishwaji rasmi zilifika tarehe 17/09/2009 kwa kufuata taratibu zote za uanzishwaji wa Tawi. Katika kikao cha 121 cha Baraza la chuo cha 29/09/2011 kiliridhia rasmi uanzishwaji wa THTU-SUA. Kwa hiyo basi menejimenti ya SUA kwa barua yake yenye Kumb. Na. SUA/CG/46 ya tarehe 03/10/2011 iliujulisha uongozi wa THTU-SUA kuwa uanzishwaji wa Tawi la THTU-SUA ni halali na hivyo kupelekea kuanza kutekeleza shughuli zake kama chama cha wafanyakazi katika taasisi hii.
HISTORIA YA THTU
Uanzishwaji wa THTU ni matokeo ya kamati za viongozi kutoka matawi ya Vyuo Vikuu vya Umma Tanzania, ambavyo vilifanya kazi kubwa kuanzia mwaka 1998 hadi 2008, lengo likiwa ni kudai maslahi bora, kuunganisha nguvu za pamoja na kuitaka Serikali yetu kuboresha mazingira ya kazi ya wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania.
Kamati za viongozi kutoka Taasisi hizo mwaka 2005 waliunda jopo la pamoja la vyama vya wafanyakazi, vyama vya kitaaluma na mabaraza ya wafanyakazi, kwa nguvu na mshikamano ndiyo iliyopelekea kuundwa kwa kamati ya Rais ya kuangalia matatizo ya wafanyakazi kutoka Taasisi za Elimu ya Juu. Huo ndio ukawa mwanzo wa kuzaliwa kwa chama cha wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (THTU).
DIRA YA CHAMA (Vision)
Kuwa chama cha wafanyakazi kiongozi Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine. Lengo likiwa kinga, kulinda na kuangalia ustawi wa wafanyakazi wakati huo kuangalia njia za kusaidia kupunguza athari za kiuchumi kwa wafanyakazi.
DHIMA YA CHAMA (Mission)
Kuunganisha wafanyakazi wote wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine katika kupigania na kujikinga na mazingira ya kazi hatarishi, ustawi na mazingira bora na wakati huo kukuza tija na huduma na ufanisi wa kazi katika maeneo yetu ya kazi.